Tuesday, October 12, 2010

Toba Za Lorot Mwana Wa Milima

Mabibi na Mabwana, wenzangu mnaonipenda na msionipenda,Wanamilima wote, nina toba. Samahani, tatu. Kumbukizi zangu zimenisakama. Nimezama katika bahari ya luja kwa takriban saa mia moja ishirini katika tafakari na tafakuri si haba. Akili zangu zaweza kuniduru. Timamu zangu zinanielemea. Naweza kujitia hamnazo kuwa sijihusishi lakini akili yangu haitaniruhusu.

Tuambiane ukweli, basi. Sitakupaka mafuta kwenye mgongo wa chupa.

Mosi, tumehadaiwa, tumedanganywa, tumetapeliwa. Uwongo tumelishwa, uwongo tusiouelewa bayana. Tumekuwa watu baki. Tumejitia hamnazo isiyo kifani. Mfano, katika lile somo la hesabu. Ulifunzwa kipengele Fulani kiitwacho inteja na namba laini. Pia, ukafunzwa ikwesheni zinazoenda sambamba ( walioenda shule watakuambia simultaneous equation). Mwalimu wako kisha akajitosa katika mambo yake ajabu ajabu kisha akakufunza concept moja kibao kinachoitwa Naotiko Mail (Nautical Miles). Na lugha moja ya wapiga ramli iitwayo matrix. Muungwana, tangu lini namba zikasimama moja juu ya nyingine ukadhani ghorofa halafu ukaiita hesabu? Makubwa haya! Dunia imepasuka mahali! Tuambiane ukweli.

Pili, kasheshe zangu zimenitia matatani. Ninapopiga soga za Milima, ninapokariri hadithi za Milima, ninapozifuma na kufumua na kuipinda na kuipindua, wengi hamnielewi. Mwazisoma tu kisha mnamaka Lorot Mwana wa Milima, haambiliki hasemeki. Hawezi akaaminika. Ni kinyonga.

Sikatai.

Nakiri mashtaka. Lakini kumbuka mwenzangu, mwana na binti wa Milima, kwamba dunia hii yetu ina kunga zake tusizozielewa. Imejipinda ajabu. Haiko laini. Lau ingekuwa laini ungenilimbikizia malalamishi yako, Muungwana. Ulimwengu ni malimwengu. Hivyo basi, ninapochukua jukumu la usanii na kuchora dira ya dunia jinsi ninavyotazama mie sifurahii hili jukumu. Linanipa jakamoyo, linanitia huzuni, majonzi na jitimai si haba. Mara si moja wakati nimejiambia kuwa nitaitupa michoro hii baharini ili iliwe na papa na nyangumi. Lakini, kwa kuponda kwa awali, ninajiambia mimi ni Msanii, nachora dunia jinsi ilivyo. Sizidishi sipunguzi. Waweza kuwa hakimu, mwana wa Adamu mwenzangu.

Lakini mimi, Lorot Mwana wa Milima, sitakuwa hakimu. Siwezi kukashifu, sitafoka, sitakaripia. Nilicho nacho ni riwaya na ngano za Milima. Zimezaliwa ndani ya mapango ya milima. Zimehifadhiwa na wanamilima kama wewe. Kinitiacho huzuni ni kwamba zimeoshwa na watu katika zumbukuku zao. Hata hivyo, mimi ni Mjumbe ninayewasilisha ujumbe kwa Wanamilima. Wanamilima wanaweza kunikashifu, kunizomea, kunifokea hata kuniua. Lakini haidhuru. Mirindimo na rungwaya za Milima zitaendelea kurindima na kupaaza sauti toka mlima mmoja hadi mwingine. Katika vikelele hivi, Lorot Mwana wa Milima, atazisikiza na kuziwasilisha jinsi zilivyo. Milima imempatia wadhifa na imani.

Tatu, na usikanganyike Mwana Milima mwenzangu: Salem Lorot Dick ( ndio hivyo tena na Majina ya Kizungu, sisemi kitu) na Lorot Mwana wa Milima ni watu tofauti kama alama nyekundu na kijani kibichi. Salem ni msiri, aliyesetiri kila kitu kilicho chake kifuani na hapendi kujitia katikati ya watu kama mchuzi katikati ya ugali. Salem amelogwa na shughuli zinazomwandama kibao. Kwa upande mwingine, Lorot Mwana wa Milima ni kinyume kabisa cha Salem. Lorot ni mcheshi, mwenye kasheshe, ni mfitini, anapenda umbeya, atakuambia mechi kati ya Iraki na Sofa Paka ilichezwa vipi mwaka wa 1981. Lorot Mwana wa Milima ana ngano si haba za Milima.

Hivyo basi, unapofura kama kaimati na kunihukumu kwamba Salem, wewe umevunja mwiko za wanamilima, huaminiki tena, umepoteza fahamu zako. Kisha, mie Lorot Mwana wa Milima nitajibu kwa Ungwana wa Wanamilima walionifunza utu na ubinadamu kuwa mimi nina heshima za Milima. Elekeza lawama kwa Lorot Mwana wa Milima, si mimi Salem. Na nikifikiria zaidi kuhusu mambo haya ninamwonea huruma Lorot Mwana wa Milima. Amesongwa na hadithi za kusononesha za Wanamilima. Uwendawazimu umesheheni kwenye milima. Anapotunga hadithi hizo basi ni mirindimo ya milima. Tutamlaumu vipi anayewasilisha ujumbe huu?

Kwa kumalizia, wanamilima, nimejieeleza bayana. Nafsi yangu imetulia. Tafakuri zangu zimenyooka. Iwapo kutakuwepo na tashwishi kuhusu nani aliyeendika ujumbe huu usichelee kusema Lorot Mwana wa Milima!

Asante Mwana Milima.

Barua Kutoka Jela: F.L.R.

Mwana wa Milima, ninaandika barua hii nikiwa jela. Hata ingawa ninaiandika katika karatasi shasha, la mno ninalokutaka radhi liwe ni ujumbe ninaowasilisha. Yapo mengi ningetaka kukuambia lakini muda na barua hii haitoniruhusu, Mwana wa Milima.

Jela inasikitisha. Mara nyingi naona heri nijitie kitanzi juu ya paa; nife Maskini aliyedharauliwa na kuonewa kero. Mara nyingine mimi hujiona nikisimama mbele ya askari na kumwambia: “Elekeza mtutu wa bunduki kwangu, nifyatue risasi, lipua ubongo wangu utawanyike mara elfu”. Na mara nyingine mimi hujipata nikitafakari jinsi ambavyo kifo changu kitapokelewa. Wafitini, wadhabidhabina na mahasidi watarusha roho zao na kuitisha karamu. Labda kifo changu kitakuwa cha kawaida. Haitatangazwa redioni wala magazetini. Labda sitazikwa. Labda kipande cha ardhi kitakosekana kwani mimi ni fedheha.

Lakini Mwana wa Milima, nakuomba usome barua hii hadi mwisho. Baada ya hapo, maadamu ni karatasi shasha waweza kuitumia msalani. Waweza hata kunifokea na kukaripia nyendo zangu. Hilo halinipigi mshipa. Cha mno hivi sasa ni kuwasilisha ujumbe huu.
Usidanganywe, Mwana wa Milima, ukiulizwa ni kipi cha kukukata maini zaidi jibu si umasikini. Jibu si mali nyingi. Jibu si njaa wala shibe. Hata jibu si elimu. Waweza kuuliza: Ni ajabu hilo, ni falsafa ipi inayokuandama?

Hii si falsafa wala zoezi la kisosholojia. Abadan! Ni mdahalo nawe Mwana wa Milima. Na chilumbo hili labda laweza kuwa la mwisho. Maisha ya jela ni upepo. Leo upo, kesho haupo umekuwa Mwendazake na kipindupindu.
Ulipozaliwa, Mwana wa Milima, ulikuwa uchi. Lakini ulikuwa huru. Ulipoendelea na maisha yako, minyororo ikakuzunguka. Wengi hunicheka. Husema: Mfungwa Maskini Mungu Amrehemu. Lakini iwapo kuna watu wanaohitaji rehema mara kumi ni ninyi mnaojigamba mko huru.
Katika jela, nimezungukwa na kuta za binadamu. Nimegubikwa na giza na harufu mbaya ya kutisha. Ninyi msio jelani mwadhani hamjazungukwa na kuta zozote wala giza wala harufu mbaya. Mmekosea! Mimi jelani niko huru akilini. Timamu zangu zinapepea katika anga za juu za Mwewe na Shomoro. Ninafikiria na kuunda mambo akilini bila kejeli wala wasiwasi. Na woga wangu nimetundika mitini, haziniandami.

Na ninyi je? Akili zenu ni finyu. Mwaogopa kufikiria. Mwapenda vya bure na vya rahisi. Njia zenu ni za mkato. Lenu ni kuiga. Akili zenu mwaiga, mienendo zenu ni za kuiga, kuongea kwenu ni kwa kuiga, mapenzi yenu ni ya kuiga. Kuta zilizowazingira ninyi zashinda hizi za jela. Japo taa zinawamulika kotekote maisha yenu ni ya giza. Kila mnakoenda mna woga. Mwaogopa kila kitu. Mwaogopa binadamu, mwaogopa kifo ilhali mwataka kwenda mbinguni, mwaogopa kuishi. Ajabu ni kwamba ninyi mwajiona mko juu, mmefura kama kaimati.

Hii ndiyo maana, Mwana wa Milima, sipati tamaa ya maisha yenu. Mmebaki vikaragosi na wanasesere. Hata nife leo, Mwana wa Milima, niko radhi kuishi katika nyendo zangu na upeo wa akili zangu kuliko majisifu na majigambo yenu yasofaidi chochote. Hata nifyatuliwe risasi jelani nitabaki mimi.
Lakini usikonde Mwana wa Milima. Japo ngano zako zitabakia ngano tu, jipe moyo. Ari, Mwana wa Milima, ipo siku inshallah, ipo siku….

Wasalimie wote,
F.L.R

Zeruzeru: Hotuba ya Lorot Mwana wa Milima

Kisha nikasimama juu ya kilima kidogo, umati mkubwa umenizingira. Wapo waliokuwa wakilia, wengine wakijibiringisha kana kwamba wamepagawa. Nilikuwa na ujumbe. Na ujumbe huo ulikuwa na uzito wake ambao kidogo singeweza kuihimili.
Kisha nikaanza usemi wangu mimi Mwana wa Milima:
“Wanamilima, nina huzuni leo. Sina ucheshi. Bashasha imeniondoka na suduri yangu ni jakamoyo na simanzi. Habari hii ni juu ya ndugu zetu zeruzeru. Mila tunayo, desturi tunazo, itikadi tumezihifadhi lakini huu uhasama juu ya wenzetu zeruzeru si mila, desturi na itikadi za wanamilima. Kamwe, ukatili juu ya ndugu zetu haioani vyema na weupe wa nyoyo zetu.
“Anapozaliwa zeruzeru, huzaliwa sawa na watoto wengine. Naomba kukosolewa ikiwa sineni ukweli. Milio yao si za nyani ama hayawani. Wao hubebwa miezi tisa kama wanamilima wengine. Wao hunyonyeshwa sawa na watoto wengine wa Wanamilima. Wao hucheza sawa na watoto wa wanamilima.
“Nao wakijikwaa hutoa damu rangi moja na Wanamilima wengine. Damu yao ni nyekundu, si buluu, kijani kibichi au hudhurungi. Nao hulia sawa na Wanamilima.
« Anapotimia umri wa kuoa, zeruzeru hupenda kama Mwanamilima yeyote yule. Anaweza kuhisi upweke ambao mapenzi huukabili. Japo ngozi yake haina rangi, zeruzeru anaweza kubaini rangi ya mapenzi na kupenda. Na anajua sikitiko na kero za mapenzi. Wapo watakaompenda, wapo watakaoidharau penzi lake, wapo watakaomzuzua na penzi vuguvugu. Lakini zeruzeru aweza kupenda na kupendwa.
« Ni ngozi yake tu iliyo tofauti. Na Maulana ndiye amemfanya hivyo. Zeruzeru katu hakuzaliwa zeruzeru kwa hiari. Asilani! Ni sawa na wenzetu wanamilima wenye vilema. Naam, maumbile ya Mola haina doa na sisi Wanamilima hatutouliza maswali.
“Ndio maana siwaelewi Wanamilima tena. Ukatili umetuingia kama pepo mchafu. Utu tumekosa. Tumekuwa hayawani. Hata afadhali hayawani kwani hayawani hupenda na kujali.
“Vipi tuwatumie ndugu zetu zeruzeru kama kafara na tambiko za kiganga?
Vipi tuwauze sawa na vitu mnadani ilhali ni wanamilima wenzetu?
Zeruzeru walitufanya nini ili tuwaue na kuwaangamiza?
Kosa lao ni lipi kuzaliwa zeruzeru?

“Wanamilima wenzangu ikiwa kuna wachawi basi ni sisi. Ikiwa kuna wauaji basi ni sisi wanamilima. Twajigamba eti sisi tuna ustaarabu na stara ilhali tunawadhulumu zeruzeru wenzetu. Zeruzeru anapovaa kofia ili kujizuia dhidi ya miale mikali ya jua tunamcheka na kumwita mzungu mchafu. Watoto wetu tukawastahimili wanapowakejeli zeruzeru. Nafasi za kazi tukawapunja hata katika nyakati ambazo zeruzeru ana shahada na taaluma katika kazi husika. Mafuta za kujipaka ili kuzuia makali ya miale ya jua bado tukaitoza ushuru na kuwaangamiza zeruzeru katika lindi la mateso. Zeruzeru akawa kama mbwa koko, hapendeki. Sawa na mnyama akawa anawindwa, kuandamwa na kuwawa. Zeruzeru akawa ametengwa na jamii ya wanamilima sikitiko lake lisiweze kusikika.
Nasi wanamilima kila siku twahubiri kuhusu haki. Tutaonekana televisheni na majukwaa ya kifahari tukikashifu na kulaani unyanyasaji na dhuluma za kila aina katika jamii ya wanamilima. Lakini jioni katika giza zeruzeru atachinjwa ili kutibu ukimwi na kufukuza mapepo. Pasi na kuangaziwa, Robinson Simiyu atahadaiwa kufunga safari kwenda Tanzania kupata ajira ya kuwa utingo ili afanywe tambiko la kiganga. Robinson Simiyu hatumpi ajira nchini. Na kama taifa la wanafiki na mafarisayo na masadukayo tutapokea habari ya kunusuriwa kwake kama mshtuko. Tutamwelekeza Robinson Simiyu mbele ya kina Paparazi ili tujiimarishe kisiasa lakini sheria ya kumlinda hatutaipitisha. Wiki mbili zikiisha tutamsahau Robinson na zeruzeru wote. Tutajishughulisha na mambo mengine za kutukera . Zeruzeru wanaweza kuangamia na kwenda kuzimu!
Ah! Wanamilima! Siwaelewi tena! Naam, zeruzeru ataendelea na maisha yake. Waweza kumdharau, kumkejeli, kumfitini, kumkebehi. Waweza kumfanya tambiko la kishirikina. Waweza kumuandama na kumchinja. Lakini ukweli utasalia kuwa zeruzeru ni binadamu kama wewe.
Wanamilima, mmenisikia mimi na nyuso zenu zaonyesha kukerwa na tukio hili. Sihitaji kero zenu, sihitaji kusikitika kwenu. Huruma haisaidii. Twaweza kufanya nyoyo zetu ziwe ngumu au twaweza kuzifanya laini ili kujenga taifa moja ambalo zeruzeru hatabaguliwa na kudharauliwa. Taifa hilo la Wanamilima ni taifa twaweza kulijenga pamoja. Itaanza kwa kubadili fikra zetu dhidi ya ndugu zetu Wanamilima: Zeruzeru.